Islamic Calender

Powered by Blogger.

MASHART YA TOBA



Mwenyezi Mungu anasema:
"Sema: Enyi waja wangu walio jidhulumu nafsi zao! Msikate tamaa na rehema ya Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu husamehe dhambi zote. Hakika Yeye ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu."
Az Zumar - 53
Hii ni rehema kubwa iliyojumuisha msamaha wa madhambi yote. Hata yawe makubwa namna gani.
Huu ni mwito kutoka kwa Muumba wa mbingu na ardhi kwa wote wenye kumuasi Mola wao, na wale waliozama na kufurutu mpaka katika maasi hata wakakata tamaa kuwa hawatoweza tena kusamehewa. Huu ni mwito kutoka kwa Muumba wa kila kitu, Mwenye kuzijua vizuri nafsi za viumbe. Mwenye kujua kuwa shetani amemkalia mja wake katika kila njia, na kwamba shetani huyo anao uwezo wa kumshinda nguvu mja masikini kwa kujipenyeza kupitia sehemu za udhaifu wake akamchezea na kumtelezesha, hasa pale mja anapoiacha kamba ya Mwenyezi Mungu akaishikilia kamba ya dunia.
Mwenyezi Mungu kwa kuuelewa vizuri udhaifu wa mja Wake, anamnyoshea mkono wa msaada na rehma, ili asikate tamaa baada ya kuzama akadhani kuwa hapana tena tumaini.
"Msikate tama."
"Hakika Mwenyezi Mungu husamehe dhambi zote. "

Ewe Mola mwingi wa kusamehe,
Niruzuku ghufurani        Niepushe na maasi
Nakuomba ya Manani    Dhamiri inanighasi
Naungua kifuani            Kama moto wa nuhasi
Rabbi nighufurie           Ewe Ghafuru Rahimu

Kheri ukinishushia         Nasahau kwa wepesi
Mitihani yanijia              Mimi nazidisha kasi
Wewe wanichukulia       Miye nazidi kuasi
Rabbi nighufurie           Ewe Ghafuru Rahimu

TOBA ZIPO AINA MBILI;
1.      Toba ya mtu aliyetenda dhambi baina yake na Mola wake.
2.      Toba ya dhambi yenye uhusiano na mwanadamu mwengine.

Mtu anapotenda dhambi baina yake na Mola wake, na dhambi hiyo ikawa haina uhusiano na mwanadamu mwengine, basi masharti ya kutubu kwake ni matatu:-
3.      Ayaache maasi hayo
4.      Ajute kwa kuyafanya maasi hayo.
5.      Atie nia ya kutoyarudia tena.
Toba ya kweli haisihi likikosekana mojawapo ya masharti hayo.

Maulamaa wanasema kuwa inamuwajibikia mtu kutubu kwa kila dhambi aliyotenda na atie nia ya kutoirudia tena.
Mtu anapomuibia mwenzake kitu, kisha akajuta na akaamua kumrudishia mwenyewe kitu chake hicho na kumuomba msamaha, je mtu huyo atakirudisha akiwa na nia ya kukiibia tena?
Bila shaka hatokuwa na nia hiyo. Na hivyo ndivyo ilivyo wakati mtu anapomuasi Mola wake kisha akajuta na akaamua kutubu, bila shaka hatotubu huku akitia nia ya kulirudia tena kosa hilo.

Masharti ya kutubia dhambi yenye kuhusiana na haki za mwanadamu mwingne, kama vile kumdhulumu au kumuibia au kumsengenya ni manne
Masharti matatu yaliyotangulia kutajwa, na la nne ni 'kuirudisha haki ya aliyedhulumiwa.'
Ikiwa ni ya kumvunjia heshima au kumsengenya, hapo litaongezeka sharti la kuomba msamaha.
Baadhi ya Maulamaa wanasema kuwa; kwa vile mambo ya kusengenya huenda yakasababisha matatizo mkubwa zaidi pale mtu anapoendewa kuombwa msamaha, basi inatosha badala yake uwe ukimuombea dua mtu huyo kila wakati na ni vizuri zaidi kama kama utakwenda katika vikao ulivyokuwa ukimsengenya ukazungumza juu ya mema yake, huku ukiwajulisha watu kuwa ulikuwa ukikosea pale ulipokuwa ukimsema vibaya.
Maulamaa wanasema kuwa mtu akifanya hivyo huenda Mwenyezi Mungu akamghufiria madhambi yake.
Wengine wakasema kuwa toba sahihi haipatikani mpaka umuendee mtu huyo na kumtaka radhi kwa maovu uliyokuwa ukizungumza juu yake.

Kwa mtu aliyemdhulumu mwenzake mali kwa njia ya hiana nk. akaona vigumu kumrudishia mwenyewe haki yake na kumuambia ukweli, basi inatosha ikiwa badala yake atanunuliwa zawadi kiasi cha thamani ya mali yake na kumpa yeye au wanawe kama zawadi bila kumjulisha sababu ya zawadi hiyo.
Na kama haiwezekani kufanya hivyo basi inatosha kuchukuwa thamani ya mali hiyo na kufanya kila hila ili uweze kuifikisha nyumbani kwake na kuiweka mahali popote, na kama hilo pa haliwezekani basi inatosha kuiweka japo ndani ya uwa wa nyumba yake au mahali popote ikiwa pana uhakika wa kumfikia mwenyewe haki yake.
Iwapo hapana njia yo yote ya kumfikishia mdhulumiwa haki yake, kwa mfano mtu huyo amesafiri na anwani yake haijulikani, au amekwisha fariki dunia na haijawezekana kumpata mrithi wake nk. basi thamani ya haki yake inaweza kutolewa sadaka kwa jina lake.
Kumbukeni ndugu zangu kuwa dhambi yoyote baina ya mtu na Mola wake inafutika, lakini baina ya mtu na mwenzake, haifutiki isipokuwa kwa mojawapo ya njia zilizotajwa au zilizo mfano wake.
Mwenyezi Mungu anasema:
"Yaendeeni upesi upesi maghufira ya Mola wenu na Pepo (Yake) ambayo upana wake (tu) ni (sawa na) mbingu na ardhi, (Pepo) iliyowekewa wamchao Mungu."
Aali Imran - 133
Na katika hadithi, Mtume wa Mwenyezi Mungu (Swalla Llahu alayhi wa sallam) amesema:
"Mwenyezi Mungu hufurahi sana kwa toba ya mja wake kuliko msafiri aliyepanda mnyama kisha mnyama wake akamuangusha na kumkimbia akiwa amebeba chakula chake na maji yake, akakata tamaa ya kumuona mnyama huyo tena, akaenda chini ya mti na kujinyosha chini ya kivuli chake, keshakata tamaa, na alipozindukana akamuona mnyama wake mbele yake na vifaa vyake kamili, kisha akasema kwa furaha (bila kujijua), 'Mola wangu, wewe ni mja wangu na mimi ni mola wako', kwa furaha nyingi akakosea."
Bukhari na Muslim
Kwa vile bado muda unao, na hujui kama muda huo utakuwa nao kwa muda mrefu au mfupi, kwa nini basi hayakimbilii maghfira ya Mola wako kabla haujafika wakati wa kujuta na majuto yasiweze kusaidia kitu?
Mwenyezi Mungu anasema:
"Au ikasema (nafsi); 'Kama Mwenyezi Mungu angeniokoa bila shaka ningekuwa miongoni mwa wenye kumcha Menyezi Mungu.'
Au ikasema ionapo adhabu; 'Kama ningepata marejeo (ya kurejea tena duniani) ningekuwa miongoni mwa wafanyao mema.'
(Ataambiwa); 'Kwa nini! Bila shaka zilikujia Aya zangu ukazikadhibisha na ukajivuna na ukawa miongoni mwa makafiri."
Az Zumar 57-59

<Source: http://groups.yahoo.com/group/jifunzeuislamu>

Comments :

0 comments to “MASHART YA TOBA”

Post a Comment

 

Website Hit